MZEE MALECELA AWAASA WATANZANIA KUJIHADHARI NA WASIOPENDA AMANI

 

Mzee John Samuel Malecela, mmoja wa viongozi waandamizi na mashuhuri katika historia ya Tanzania, ameendelea kuwa kielelezo cha busara na hekima kwa Taifa. Amezaliwa miaka 91 iliyopita katika kijiji cha Bugiri, mkoani Dodoma, na mchango wake katika siasa, diplomasia, na uongozi wa umma umeacha alama isiyofutika.

 

Katika maisha yake ya utumishi kwa Taifa, Mzee Malecela aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali zenye uzito mkubwa serikalini. Alianzia katika nafasi ya Balozi wa Tanzania nchini Uchina, kisha akateuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje, na hatimaye akawa Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Safari yake ya uongozi ni somo tosha kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

 

Ziara ya Machifu na Ujumbe wa Busara

Tarehe 7 Juni 2025, Mzee Malecela alipokea ugeni wa heshima kutoka kwa Machifu wanaowakilisha mikoa tisa ya Kanda ya Kusini ya Vita ya Majimaji – Rukwa, Songwe, Ruvuma, Njombe, Mbeya, Iringa, Morogoro, Lindi na Mtwara. Ziara hiyo iliratibiwa na muunganiko wa taasisi mbili: Akida Wabu Foundation ya Ruvuma na Chifu Kapere Foundation ya Rukwa.

 

Machifu hao walimtembelea nyumbani kwake, Uzunguni jijini Dodoma, kwa lengo la kumjulia hali, kumwombea pamoja na kulibariki Taifa na uongozi wake. Mzee Malecela, kwa hekima yake ya miaka mingi, alitumia fursa hiyo kuwasilisha ujumbe muhimu kwa Taifa zima, hasa tunapoelekea katika Uchaguzi Mkuu.

 

Aliwaasa Watanzania kuendelea kulinda amani kwa gharama yoyote, akisisitiza kuwa kuna hatari kubwa ya kuruhusu chuki na migawanyiko kuota mizizi. Aliwakumbusha madhila yaliyotokea nchini Rwanda wakati wa vita vya Wahutu na Watusi, akisema:

 

"Ukitaka kukarabati nyumba, usivunje msingi wake."

Kauli hii inaashiria umuhimu wa kufanya maboresho ya Kitaifa bila kuharibu misingi ya amani, umoja na mshikamano wa Kitaifa.

 

Ujumbe kwa Taifa Mzee Malecela alihimiza utekelezaji wa miradi ya maendeleo uende sambamba na utunzaji wa maadili, utu na mshikamano. Alisisitiza kuwa mafanikio yoyote ya kiuchumi au kisiasa hayawezi kuleta manufaa ya kweli iwapo nchi haitadumisha amani, ambayo ndio msingi wa maendeleo endelevu.

 

#KhomeinTvUpdates 

 

✍️Mwandishi wetu

 

PIA USIACHE KU SUBSCRIBE

CHANEL YETU Khomein TV

YOUTUBE UWE WA KWANZA 

KUFIKIWA NA HABARI ZETU

 

Follow Insta & Threads @khomeintv_

Tufollow pia kwenye X (Twitter), TikTok

@khomeintv na Facebook Khomein Tv

Post a Comment

0 Comments